SBL Yafungua Ghala Mbeya
Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) imefungua ghala lake kubwa la kwanza
Mkoani Mbeya lenye uwezo wa kuhifadhi masanduku 80,000 mpaka 100,000 ya
bia kwa ajili ya kuhifadhi na kusambaza bidhaa zake kwa wateja wake wote
wa ndani na nje ya nchi.
Hayo
ni mafanikio makubwa kwa SBL yaliyopatikana hivi karibuni katika nusu
ya kwanza ya mwaka 2014. Ufunguzi wa ghala hilo utaleta mafanikio
makubwa katika uendeshaji wa shughuli za SBL pamoja na kugusa maisha ya
watu waliopo katika shughuri mbalimbali za uendeshaji wa SBL.
Mkurugenzi
Mtendaji wa SBL, Bw. Steven Gannon alisema ghala hilo litaongeza uwezo
wa kampuni kuzalisha bidhaa zake kwa wingi kwa wateja wake wa mikoa ya
nyanda za juu kusini ambayo ni Mbeya, Rukwa, Iringa na Ruvuma. Ghala
hilo litasaidia kuweka akiba ya kutosha ya bia tofauti na hapo awali.
“Katika
msimu huu wa Siku Kuu ya Krismasi na Mwisho wa Mwaka tunauhakika wa
kukidhi mahitaji ya wateja wetu. Kila mtu atakunywa mpaka atakaporidhika
na kwa ustaarabu,’’ alisema Bw. Gannon.
“Ufunguzi
wa ghala hilI kwa kiasi kikubwa utapunguza gharama za usafirishaji kwa
upande wa wasambazaji wetu na kuongeza manunuzi zaidi. Hii itapunguza
gharama zao za muamala na hivyo kupata faida zaidi kwa kushirikiana na
SBL,” aliongeza kusema Bw. Gannon.
Ufunguzi
wa ghala hilo pia utatoa fursa zaidi za ajira katika nyanja mbalimbali
za shughuli za SBL kama vile madereva, mafundi magari, mamalishe,
makarani na kuongeza idadi ya wasambazaji.
“Matokeo
ya mwisho ambayo ni muhimu zaidi kuliko yote kwa kufunguliwa ghala hili
ni kuongezeka kwa mauzo kwa kampuni ya SBL, kwani wasambazaji zaidi
kutoka nyanda za juu kusini watavutiwa kujiunga na biashara yetu
kutokana na upatikaji huduma hiyo kwa urahisi,” alisema Bw. Gannon.
Mafanikio
mengine ya SBL ni kwamba Novemba 23, 2014 walisherehekea kutimiza siku
ya 1000 bila kupata ajali katika kiwanda cha SBL cha Mwanza, ambapo hiyo
ni rekodi ya kwanza kuwekwa Tanzania na ya pili kwa Diageo.
Naye
mgeni rasmi, Norman Sigalla alisema ufunguzi huo ni hatua muhimu
katika juhudi za kampuni ya SBL ya kuleta huduma zake karibu na wateja
wake. Alisema hiyo ni hatua muhimu kwa watumiaji wa bidhaa hizo katika
mikoa ya Nyanda za Juu kusini kwani sasa kutakuwa na upatikanaji wa
uhakika na kwa muda wowote wa bidhaa za SBL.
Bw.
Sigalla alisema Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini itanufaika na ufunguzi
huo kwa sababu mawakala wa bidhaa za SBL walikuwa wanalazimika kwenda
umbali mrefu kutafuta bidhaa hizo hivyo kuwaongezea gharama za
uendeshaji. Jambo hilo lilipunguza sana soko la bidhaa za SBL katika
maeneo hayo.
Mkuu
wa Wilaya alisema kitendo hicho kilimnyima mteja/mnywaji haki yake ya
msingi ya kuchagua kinywaji akipendacho, kwani alilazimika kunywa kile
kinachopatikana kwa wakati huo.
Bw.
Sigalla alisema Serikali inatambua mchango mkubwa utolewao na SBL kwa
wakulima wa shayiri na mahindi katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini,
akisema kwa kuingia nao mikataba ya kununua mazao yao wanafaidika kwa
namna nyingi.
Alisema
kipato cha uhakika wanachopata kutoka SBL kinawawezesha wakulima hao
kumudu gharama mbalimbali za maisha kama vile kulipa karo za watoto wao
wanaosoma, kulipia huduma za hospitali na mahitaji mengine muhimu.
Mkuu
huyo wa Wilaya aliuomba uongozi wa SBL kufikiria kujenga kiwanda mkoani
Mbeya ili kuongeza kasi ya ukuaji uchumi na kuongeza ajira kwa watu
wenye sifa katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.
No comments:
Post a Comment